Thursday 27 October 2016

WAKAZI TEGETA WAHOFIA “UGOGONI” KURUDI


Na Agustino Luambano.                                                         
Baadhi ya wakazi wa kata ya Kunduchi Tegeta jijini Dar es salaam wameonesha wasiwasi wao juu uwezekano wa eneo lililotumiwa kibiashara linalojulikana kama “Ugogoni” kuendelea tena na shughuli zake zilizokuwa zinafanywa hapo  awali licha ya jeshi la polisi kulizuia na kubomoa eneo hilo.
Eneo hilo lililokuwa likihusisha biashara ndogondogo kama vile; vinyozi, mama rishe, pombe za kienyeji na pombe hatari ya gongo lilizuiwa na kuvunjwa na jeshi la polisi baada ya wakazi wa eneo hilo kulalamika kuibiwa mali zao na vijana waliokuwa wanashinda eneo hilo mchana kutwa wakisingizia kufanya biashara katika eneo hilo.
Wakitoa malalamiko yao kwa nyakati tofauti tofauti baadhi ya wakazi wa karibu na eneo hilo ambao hawakutaka kutajwa majina yao walidai kuwa licha ya jeshi la polisi kuwaondoa wafanyabiashara wa eneo hilo na kubomoa vibanda vyao kwa zaidi ya miezi sita iliyopita, bado imeonekana kuwa kuna baadhi ya vijana ambao wanaonekana kukaa katika vichaka vya eneo hilo ambalo kwa sasa  ni kama msitu.
Fred Msungu ambaye hakutaka kueleza cheo chake licha ya kuonekana kuwa na uongozi katika eneo hilo alieleza kuwa “kilichowatoa watu hapa ni uuzaji wa gongo, kuvuta bangi, ukahaba, na wizi. Hapa ilikuwa hakatizi mtu bila kuibiwa” Alisema Fred.
Aidha Bwana Fred aliongeza kuwa “baada  ya polisi kuwaondoa watu na kuvunja vibanda hapa, amani ilikuwepo na matukio ya wizi yalitulia lakini sasa matukio hayo yameanza upya na bado tunawaona watu wametulia pale Ugogoni wanafanya nini?” Alihoji Bwana Fred Msungu.
Wakati wa mchana walionekana vijana wachache  wakiwa wamepumzika katika eneo hilo ambalo kwa sasa ni eneo la wazi mali ya manispaa ya Kinondoni.Vijana hao ambao hawakutaka kuhojiwa inadaiwa kuwa wakati wa usiku  wanaongezeka na kufanya uhalifu.

No comments:

Post a Comment